WAZEE, WALEMAVU, WENYE MAHITAJI 6,000 WAPEWA BIMA YA AFYA NA DKT. TULIA

Rais wa Umoja wa Mabunge Duniani (IPU) na Spika wa Bunge Dkt. Tulia Ackson amefanya tukio la kihistoria katika Mkoa wa Mbeya baada ya kutoa bure kadi za bima kwa kaya 1,000 zenye watu 6,000.
Dkt. Tulia ambaye pia ni Mbunge wa Jimbo la Mbeya mjini ametoa bima hizo ikiwa ni mwendelezo wake wa awamu ya tano ya kusaidia wahitaji kwenye makundi ya walemavu, wazee na wenye mahitaji maalum.
Katika hafla hiyo iliyofanyika katika viwanja vya stendi ya mabasi kabwe , Mgeni Rasmi alikuwa Naibu Waziri wa Nishati Dkt. Dotto Biteko sambamba na watendaji wa Serikali na Chama.
Akizungumza na maelfu ya wananchi Dkt. Tulia amesema huo ni mpango endelevu wa kutoa bima za afya bure kwa wahitaji na kwamba ni kutokana na uwekezaji mkubwa wa huduma za afya uliofanywa na Rais Samia Suluhu Hassan.
“Hii ni awamu ya tano Taasisi ya Tulia Trust inatoa bima za afya bure kwa wahitaji na huu ni mpango endelevu tutaendelea kutoa kwani wahitaji bado ni wengi lengo ni kuona jamii inakuwa na afya njema” amesema.
Dkt. Tulia amesema kuwa katika Hosptali ya Kanda Serikali imewekeza kwa kiwango ikiwepo miundombinu ya majengo sambamba na vifaa tiba jambo ambalo limesaidia wagonjwa waliokuwa wakipewa rufaa kutibiwa ndani ya Mkoa.

“Miaka ya nyuma wagonjwa waliokuwa wakipewa rufaa walikuwa wakisafirishwa lakini sasa huduma zote zinapatikana katika hosptali yetu ya Kanda na bado tunaendelea kupokea fedha kwa ajili ya kuendeleza huduma ikiwepo za wagonjwa wa dharura sambamba na vituo vya afya na zahanati” amesema.

Kwa upande wake, Naibu Waziri Mkuu na Waziri wa Nishati, ameagiza  Wizara ya afya, Hosptali, vituo vya afya na zahanati kuboresha na kuyasimamia madirisha ya wazee nchini.

Amewataka watoa huduma wasiwavunje Moyo wazee wanapofika kupatiwa huduma kwa kutambua kuwa ndio wamelifikisha taifa hapa lililo kwa ushirikiano na mshikamano.

Katika hatua nyingine amesema kama wabunge kitendo alichokifanya Dkt. Tulia kimewapa darasa kwa kutoa bima za afya kwa kaya 1,000 zenye watu 6,000.

Naye, Waziri wa Maji Jumaa Aweso amechangia Sh 10 milioni kwa ajili ya kuendeleza mpango wa utoaji za  bima za afya  kwa wananchi wa jimbo la Mbeya kupitia Taasisi ya Mbunge wa Mbeya mjini, Spika wa Bunge na Rais wa Umoja wa Mabunge Duniani (IPU).

Amesema kitendo anachofanya Dkt. Tulia anawapa somo kwani amekuwa ni Mbunge anayejua anafanya nini licha ya kuwa kiongozi mkubwa kwenye dunia lakini kila akija ziara Mkoa wa Mbeya lazima anamkuta na anaeleza matatizo ya wananchi wake.

Kwa upande wake Mratibu wa zoezi la ugawaji wa bima za afya, Frank Kalinga amesema kwa kipindi cha miaka mitano wametoa bima za afya kwa kaya 2,670 zenye wahitaji 16,020 katika Mkoa wa Mbeya.

Amesema bado mahitaji ni makubwa na kumuomba Mkurugenzi wa Taasisi hiyo kuona namna katika awamu nyingine kuzifikia kaya nyingine zenye uhitaji.

Mnufaika wa mpango huo, Fredy Pondo ameshukuru Taasisi ya Tulia Trust kwani imeweza kuthamini maisha ya wananchi wa kipato cha chini kuwapatia bima za afya zitakazo wasaidia kupata huduma za afya bure.

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *

DONATE

Give us a call or fill in the form below and we'll contact you. We endeavor to answer all inquiries within 24 hours on business days. DONATE BY BANK: Account Name: TULIA TRUST Account Number: 0150226766000 Bank Name: CRDB